Tuesday, October 13, 2015

BAADA YA UHAKIKI WATU 7,743 KUTOPIGA KURA HUKO ZANZIBAR

Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar Mh. Jecha Salim Jecha akiwasilisha Taarifa kuhusu maandalizi ya uchaguzi Mkuu 2015


Zanzibar: Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) imesema mchakato mzima wa kuhakiki taarifa katika Daftar la Kudumu la wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktobar 25 mwaka huu 2015 umeshakamilika huku watu 7,743, watakosa nafasi ya kupiga kura kwa kukosa sifa.
Akitoa taarifa ya maandalizi ya uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu 2015 kwa wadau wa uchaguzi Zanzibar Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Jecha Salim, huko katika ukumbi wa Bwawani Hotel Mjini Unguja, amesema kuwa mchakato wa kuhakiki taarifa za wapiga kura umeshakamilika baada ya kukamilika kwa uandikishaji wapya katika Daftari hilo.
Jecha alisema kuwa jumla ya wapiga kura 503,860, wametimiza masharti kuwa wapiga kura katika Uchaguzi Mkuu Mwaka huu, huku watu 7,743 wamefutwa katika Daftar la wapiga kura kutokana na kukosa sifa za kuwamo katika Daftari hilo.
“Kwa sasa hatua kubwa za utayarishaji na uchambuzi juu ya Daftari la wapiga kura zimekamilika ambapo jumla ya wapiga kura 503,860 watapata nafasi ya kuchagua viongozi wawatakao na 7,743, watakosa nafasi ya kuchagua kwa mwaka huu kutokana na kukosa sifa kisheria”alisema Jecha.
Hata hivyo Jecha alisema kuwa Tume ya Uchaguzi kwa sasa imekamilisha uchapishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura, ambapo ni matarajio yao kuwa kuanza kulibandika katika vituo vyote vya Unguja na Pemba.
Alifahamisha kuwa kazi ya ubandikaji wa majina yaliomo katika daftari hilo Tume ya Uchaguzi imepanga kuanzia tarehe 18 Oktoba 2015 kwa ajili ya kuwapa nafasi nzuri wananchi ili waweze kutazama majina yao kwa utulivu.
Jecha alisema kuwa jumla ya maeneo ya uchaguzi 380 pamoja na vituo 1,580 vya uchaguzi vinatarajiwa kubandikwa majina hayo ambapo kila kituo cha kupigia kura kitakuwa na wapiga kura 350.
“Wastani wa wapiga kura kwa kila kituo 350 ila katika mazingira maalum baadhi ya vituo vinaweza kuzidi kufikia 399, na kwa vyovyote vile hakutakuwa na kituo kitakachokuwa chini ya idadi ya wapiga kura 50”alisema Jecha.
Aliongezea kwa kusema kuwa “Tumetoa taarifa kwa kila Chama Cha Siasa kilichoweka mgombea wa Urais, kuja kuchukua Daftari hilo la wapiga kura kwa ajili ya kutumia siku ya uchaguzi kwa kuwapa mawakala wao”.
Jecha alisema kuwa kwa upande wa Tume ya Uchaguz hivi sasa mambo mengi tayari wamekamilisha ikiwamo vifaa vya kupigia kura pamoja na miongozo, kanuni na maadili ya Uchaguzi.
Kwa upande matayarisho ya upigaji kura Jecha alisema kuwa Tume imepanga kusambaza vifaa vya Uchaguzi siku ya tarehe 24 / 10/ 2015 kuanzia saa nane mchana kwa vituo vyote vya Uchaguzi,usambazaji ambao utafanywa kati ya viongozi wa tume na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
Alifahamisha kuwa siku ya upigaji kura vituo vitaanza kufunguliwa saa moja kamili (1.00) asubuhi na kufungwa saa kumi jioni (10:00) ya siku hiyo hiyo ya tarehe 25 ya Oktoba 2015.
Baada ya hatua hiyo kitakachofuata ni uhisabuji wa kura za wagombea ambapo Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo atafanya majumuisho ya kura ndani ya Jimbo na mara baada ya kukamilika Msimamizi huyo atatangaza matokeo ya Uchaguzi kwa ngazi ya Mwakilishi na Udiwani tu.
Huku matokeo ya Urais Msimamizi huyo wa Uchaguzi Jimbo atafanya majumuisho ya kura na atabandika nakala ya matokeo hayo katika ukuta ili wananchi wapate nafasi ya kuona matokeo hayo.
“Mara baada ya kukamilika kwa majumuisho Msimamizi wa Uchaguzi atampatia kila Wakala fomu moja ya mtokeo husika, huku Tume ya Uchaguzi ikibaki na kazi ya kutangaza matokeo ya Uchaguzi kwa kila Jimbo mara baada ya kufanyiwa uhakiki wa matokeo kutoka kwa wasimamizi Uchaguzi” alisema.
Jecha alisema kuwa karatasi za kupigia kura zitakazotumika katika Uchaguzi wa mwaka huu 2015 zimechapishwa kutoka nchini Afrika ya Kusini chini ya kampuni ya Bidvest-Lithotech.
Harakati zote zinazofanywa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ya uendeshaji wa Uchaguzi mwaka huu zipo chini ya Mfuko wa Serikali ya Zanzibar ambapo mwaka huu Serikali imetenga jumla ya shilling bilioni 7.5, ambapo hadi sasa Tume imeshaingiziwa shilling bilioni 2.5.

No comments:

Post a Comment